Home » » Kata ya Makurugusi yaunda vikundi vya kuzuia ajira za watoto migodini

Kata ya Makurugusi yaunda vikundi vya kuzuia ajira za watoto migodini

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Geita.

Kata ya Makurugusi iliyopo katika Wilaya ya Chato, mkoani Geita imeunda vikundi mbalimbali vinavyofanya kazi katika maeneo ya migodi ili kuzuia ajira za watoto walio chini ya umri wa miaka 18 kufanya kazi katika migodi hiyo.

Hayo yamesemwa na Afisa Mtendaji wa Kata hiyo, James Masai alipokua akiongea na waandishi wa habari juu ya Mradi wa Uondoaji Ajira Hatarishi na Vitendo vya Ukatili kwa Watoto unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD) na kuratibiwa na shirika la plan International ulivyowasaidia wananchi wa kata hiyo.

Masai amesema kuwa shughuli za maendeleo zinazofanywa na shirika hilo katika kata anayoiongoza zimeleta maendeleo makubwa hasa kwenye suala la uondoaji wa ajira za watoto katika migodi kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali kuhusu athari za ajira hizo.

“Katika Kata hii tumebahatika kuwa na vituo viwili vya migodi ambavyo hapo mwanzo watoto wengi walikua wakifanya kazi ili kujipatia vipato lakini baada ya shirika hili kutoa mafunzo yanayohusu athari za ajira kwa watoto kwa kila kijiji, tukaamua kuunda vikundi katika migodi hiyo ili kukomesha kabisa suala hili”, alisema Masai.

Amefafanua kuwa baada ya kupatiwa elimu na shirika la Plan International waliweza kuunda vikundi ndani ya migodi hiyo vikiwemo vya kamati za ulinzi, kamati za kutetea haki za binadamu pamoja na kamati za utawala ambazo zinasaidia kuhakikisha usalama wa migodi ikiwa ni pamoja na kuzuia ajira za watoto katika migodi hiyo.

Aidha, ameishukuru Serikali kwa uamuzi wake wa kutoa elimu bure kwani hapo mwanzo watoto walikua wakifanya kazi migodini kwa ajili ya kutafuta fedha za kuwawezesha kulipia ada hivyo, elimu bure imewasaidia watoto wengi kuachana na ajira za migodini na kurudi shuleni.

Naye Mchimbaji wa madini, Samson Marwa amesema kuwa kwa sasa wanaelewa athari za ajira kwa watoto hivyo wanashirikiana na wananchi kwa hali na mali kuhakikisha kuwa hakuna mtoto anayefanya kazi katika mgodi huo.

“Sisi wachimbaji wa madini tunashirikiana na wananchi katika kuzuia ajira za watoto katika mgodi wetu, tunashukuru kwa kuwa tumeweza kuzuia ajira hizo na mpaka sasa hakuna mtoto yoyote anayefanya kazi mgodini hapa”, alisema Marwa.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa