Home » » Waziri afichua siri ya walimu kukimbia vijijini

Waziri afichua siri ya walimu kukimbia vijijini

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Halima Mlacha, Dodoma.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) anayeshughulikia Utumishi na Utawala Bora, Selemani Jafo
NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Selemani Jaffo amewataka viongozi wa ngazi mbalimbali nchini kuacha kuwasaidia walimu wanaopangiwa maeneo ya vijijini kukimbia maeneo hayo na kuhamishiwa mijini. 
 
Jaffo alisema tabia hiyo imeshamiri na kuisababishia Wizara yake na ile ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kupata tatizo kutokana na walimu wengi kukimbia vijijini na kuwakosesha wananchi wa maeneo hayo huduma bora ya elimu.

Alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Geita Mjini, Kanyasu John (CCM), aliyetaka kufahamu Serikali ina maelekezo gani kwa walimu wapya ili waendelee kubaki vijijini walikopangiwa badala ya kukimbilia mijini.

Akijibu swali hilo, waziri huyo alikiri siku chache zijazo Serikali itatangaza ajira za walimu wapya na kuwapangia maeneo ya kazi. Hata hivyo, alisema katika ajira hizo za walimu kuna mikoa takribani sita lazima ipewe kipaumbele kutokana na kukabiliwa na changamoto kubwa ya walimu.

Alitaja baadhi ya mikoa hiyo kuwa ni Kigoma, Rukwa, Katavi na Geita ambako alisisitiza kuwa Serikali itatoa maelekezo maalumu kwa walimu wapya watakaopangiwa katika mikoa hiyo.

“Moja ya maelekezo kwao ni kwamba wakifika katika mikoa hiyo ni lazima waende katika maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa wa walimu. Bahati mbaya suala linalojitokeza inawezekana kabisa nyie waheshimiwa walimu wengine wakipelekwa kule mnawapa vimemo warejeshwe mijini, hali hii inasababisha maeneo ya vijijini kukosa walimu,” alisema Jaffo.

Katika swali la msingi la Kanyasu, alitaka kufahamu ni kwa nini shule ya msingi ya wasichana Nyankumbo iliyojengwa chini ya mrafi wa Geita Gold Mine imebaki kuwa ya kutwa badala ya bweni kama mpango wa awali ulivyokuwa kutokana na mazingira ya wilaya ya Geita.

Akijibu swali hilo, Jaffo alisema taratibu zinazotumika kuisajili shule kuwa ya bweni ni kwa halmashauri yenyewe kuwasilisha maombi Wizara ya Elimu kupata kibali.

Chanzo Gazeti la Habari leo
 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa