Home » » Matukio mengi ya ukatili dhidi yao yamekuwa yakifanyika ama shuleni au nyumbani

Matukio mengi ya ukatili dhidi yao yamekuwa yakifanyika ama shuleni au nyumbani

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

indexNa. Immaculate Makilika, MAELEZO
Utafiti ulofanywa mwaka 2009 na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa masuala ya watoto hapa nchini ulionyesha  kuwa kuna kiwango kikubwa cha ukatili dhidi ya watoto.
Hata hivyo, pamoja na kuwa ni utamaduni wa kigeni kuripoti matukio mbalimbali kupitia namba za simu na kwenye mitandao, matumizi ya namba 116 (Child helpline) hapa nchini yamesaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa taarifa za  ukatili dhidi ya watoto.
Kama anavyoeleza Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Mtoto kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Bwana. Benedict Missari kuanzia mwezi Juni 2013 hadi mwezi Juni 2014, Wizara hiyo ilipokea  jumla ya simu  16000 kati ya hizo1659 zilielezea ukatili dhidi ya watoto.
Kati ya simu hizo 1659, “simu 107 zilikuwa za ‘physical violence’, 23 za ubakaji, 23 za unyanyasaji mwingine wa kingono, 69 ni za kutelekezwa, 6 za utekwaji wa watoto, 12 zilihusu mimba kwa watoto huku 21 ni za uuzwaji wa watoto kwenda maeneo mbalimbali mfano Zanzibar na nchi za Uarabuni”.
 Watoto walio na umri wa chini ya miaka 18 nchini Tanzania ni sawa na asilimia 51 ya jumla ya idadi ya wananchi wote nchini.
Matukio mengi ya ukatili dhidi yao yamekuwa yakifanyika ama shuleni au nyumbani yakiwemo ya kubakwa, kukeketwa, kutelekezwa, kuchomwa moto, kutumikishwa kazi chini ya umri mdogo pamoja na ukatili mwingine wa aina hizo ambao huathiri maendeleo ya mtoto. 
Ili kukabiliana na hali hiyo, mnamo tarehe 3 Januari, 2013 Serikali chini ya  Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na Asasi isiyokuwa ya Kiserikali ya C-Sema chini ya Child Helpline International(CHI) ilianzisha na kuendesha mtandao wa mawasiliano ya simu katika maeneo ya majaribio (Pilot Areas) katika wilaya sita ambazo ni Wilaya/Manispaa za Temeke, Magu, Bukoba Vijijini, Musoma Mjini, Kasulu na Hai ili kupata taarifa za ukatili wa watoto kwa kupiga simu bure kwa kutumia namba 116(Child helpline).
Mtandao huo wa mawasiliano  unatoa fursa kwa watoto na au watu wazima kwa niaba ya watoto kutoa taarifa za ukatili unaofanywa kwa watoto katika eneo fulani ili kuwezesha wahusika kufuatilia kwa karibu na kutoa msaada kwa mtoto/watoto waliofanyiwa vitendo vya ukatili kwa kuwachukulia hatua wahusika wa vitendo hivyo vya ukatili.
Kupokelewa kwa taarifa ukatili dhidi ya watoto kumeweza kufanyiwa kazi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo makampuni ya simu kwa kumwezesha mtoa taarifa kupiga simu hiyo bure, Polisi kwenda kukamata wahusika na kuwafikisha sehemu husika kulingana na Sheria na taratibu za nchi,  na hospitali kutoa huduma kwa wahusika wa matatizo mbalimbali yanayohitaji huduma  za  kiafya.
Kuhusu uelewa wa wananchi juu ya matumizi ya simu 116 (Child helpline), kuripoti taarifa za ukatili kwa watoto katika maeneo yao, Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Mtoto, anasema wananchi wa Wilaya zile sita zilizo kwenye mradi wa majaribio (Wilaya/ Manispaa za Temeke, Magu, Bukoba Vijijini, Musoma Mjini, Kasulu na Hai) wameonyesha  uelewa wa kutosha na wamekua watumiaji wazuri tu wa namba hiyo. Hali hii imepunguza vitendo vya ukatili dhidi ya watoto katika maeneo yao.
Anataja sehemu ambazo kumekua na changamoto ya matumizi ya simu katika Wilaya hizo teule kuwa ni hasa zile sehemu za ndani zaidi ama vijijini na kusema bado kupitia wadau mbalimbali wameweza kusaidia watoto wanaokutwa na ukatili dhidi yao.
“Kumekuwa na uelimishwaji hadi ngazi ya kata na mtaa  juu ya kuripoti taarifa za ukatili dhidi ya watoto pamoja na ushirikiano wa kazi  wa karibu kati yao na maafisa maendeleo ya jamii na wadau wengine wakiwemo Wanasheria, Maafisa Ustawi wa Jamii, Halmashauri za Wilaya pamoja na Taasisi za Elimu.”Anasema Missari.
Mpango wa kuripoti taarifa za ukatili dhidi ya watoto umekuwa na mafanikio mengi ikiwemo, kusaidia watuhumiwa wa watoto waliopata madhara mbalimbali kutokana na ukatili dhidi yao kufikishwa katika vyombo vya sheria mfano wa kesi ya hivi karibuni ya mtuhumiwa aliyembaka mtoto alihukumiwa kwenda kifungo cha miaka 30 gerezani na mtoto aliyetoroshwa toka Musoma kuweza kurudishwa kwa wazazi wake.
 Bwana Missari anasema “mfano tulipata taarifa kutoka kwa jirani kuwa mtoto Nasra ameafanyiwa ukatili kwa kuwekwa ndani ya boksi kwa muda wa miaka minne huko mkoani Morogoro. Taarifa hizo tulizifanyiakazi na kufanikiwa kumpeleka mtoto kutibiwa katika hospitali ya Taifa Muhimbili. Bahati mbaya mtoto Nasra alifariki dunia Juni mosi mwaka 2014.”
Mtoto Shabani Abdalah mwenye umri wa miaka 12 anayesoma darasa la tano katika shule ya Msingi Temeke katika Manispaa ya Temeke jijini Dar salaam ameeleza namna alivyosaidiwa na matumizi ya namba 116.
“Kwa vile nilisikia shuleni kuhusu namba 116, niliamua kupiga simu na kuwaeleza namna ambavyo mlezi wangu ananitesa kwa kunifanyisha kazi ngumu, kuninyima chakula na kunipiga mara kwa mara, nafurahi kwani nilipata msaada na aliacha kunifanyia vitendo hivyo”
Pamoja na hayo, fanikio kubwa kabisa la matumizi ya namba 116 katika kuripoti taarifa za ukatili dhidi ya watoto ni kuanzishwa kwa ‘One Stop Centre’ iliyopo katika hospitali ya Amana wilaya ya Ilala mahali ambapo mtoto aliyefikwa na tatizo la ukatili hukuta huduma zote mahali pamoja kwa maana ya polisi, mwanasheria, daktari pamoja maafisa maendeleo ya mtoto.
Pia, kumekuwapo na mafunzo kuhusiana na sheria za mtoto na namna ya kulinda mtoto ikiwa ni sambamba na kuanzishwa kwa dawati la mtoto katika vituo vya polisi sehemu mbalimbali nchini.
Pamoja na mafanikio, Mkurugenzi  Msaidizi Maendeleo ya Mtoto Missari anasema kwamba baadhi ya changamoto zilizojitokeza katika kuendesha mtandao huu ni pamoja na kupokea simu kutoka karibia mikoa yote ya nchi tofauti na matarajio na maandalizi yetu ya kupokea simu kutoka kwenye wilaya ambazo zina mfumo wa ulinzi na usalama wa mtoto.
Tatizo la baadhi ya wilaya na Kata kutokuwa na maafisa ustawi wa jamii au mfumo wa ulinzi na usalama wa mtoto. Hili swala linatusababisha kupata kigugumizi pale ambapo unahitaji kufanya rufaa ya kesi kwa maafisa ustawi wa jamii kwa msaada zaidi, kwani kwa mujibu wa sheria ya mtoto ya mwaka 2009, maafisa ustawi wa jamii ndio wanajukumu la kuhakikisha usalama na ustawi mzuri wa mtoto na kuhakikisha watoto wote wanaishi katika mazingira rafiki na salama.
Changamoto nyingine ni uhaba wa wafanyakazi wa kupokea simu hizo hasa wakati wa usiku lakini pia kukosekana ‘call centre’ za kutosha kuhudumia nchi nzima pamoja na uelewa mdogo wa wananchi dhidi ya mtandao.
Uanzishaji wa Mtandao wa Mawasiliano wa Kusaidia Watoto ni mojawapo ya utekelezaji wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa  Haki za Watoto (The UN Convention on the Rights of the Child – UN CRC) ambao Tanzania  iliusaini na kuuridhia mara baada ya kupitishwa kwake.
Kwa kiasi kikubwa kama mtandao utatumiwa kwa malengo haya, ni imani yangu kuwa itasaidia kupunguza ukatili dhidi ya watoto na vile vile kuhakikisha kuwa watoto wanapata msaada stahiki na kwa wakati.
Kwa bahati mbaya watoto kama Ndyimiake Kiswigo mwenye umri wa miaka tisa anayesoma darasa la pili na Subilaga Kiswigo mwenye umri wa miaka nane anayesoma darasa la kwanza wote katika shule ya Msingi Chemuchemu katika Manispaa ya Iringa mjini, mkoani Iringa wanasema hawajui chochote kuhusu namba 116, licha ya kuwa wanasikia watoto wenzao wakifanyiwa vitendo vya ukatili katika mazingira yao.
Pia, mtu kama Avelina Mushi mwenye umri wa miaka 60, mkazi wa Kibosho Kirima mkoa wa Kilimanajro, wilaya ya Moshi vijijini, anasema hawajawahi kusikia namba 116 kuhusu kutoa msaada kwa watoto, lakini anaipongeza Serikali kwa juhudi hizi za kutafutia ufumbuzi tatizo la ukaliti na unyanyasaji kwa watoto, huku akiitaka itoe elimu kwa wananchi wengi kuhusu matumizi ya namba hiyo ili waweze kuwaokoa watoto katika matatizo mbalimbali.
Child Helpline International (CHI) ni Shirika lisilo la Kiserikali linalojihusisha na uanzishaji wa mitandao ya mawasiliano ya kusaidia   watoto. Tanzania ni moja ya nchi zinazotumia mitandao yenye kuhudumia watoto zikiwemo Afrika ya kusini, Kenya na Swaziland

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa