Home » » UJINGA NI UMASKINI TOSHA USIPOBADILIKA

UJINGA NI UMASKINI TOSHA USIPOBADILIKA

 
 Nawakumbuka wapigania haki wa Kiafrika waliowahi kuliongoza ama kulitakia mema bara hili kwa uwezo wao. Watu hawa waliongoza mapambano ya kumfanya Mwafrika awe mtu halisi, wakielewa hatari ilikuwa vipi siku ile mwanakondoo alipokutana na mbwamwitu.
Alipokwenda mtoni kunywa maji, mbwa mwitu alichanganyikiwa kumwona mwana kondoo mweupe aliyenona akiwa mbele yake. Alibubujikwa na udenda wa uchu huku akimtafutia staili ya kumla ili ladha yake isipungue badala ya kuongezeka. Akamwita: “We pumbavu njoo hapa!” Maskini mwana kondoo asiyejua uadui alimkimbilia, akamwangukia miguuni na kumwamkia “Shikamoo babu”
Mbwamwitu alifoka: “Watoto wa siku hizi hamna adabu! Kwa nini unachafua maji hadi mimi mkubwa wako nashindwa kuyanywa?” Mwana kondoo akajibu, “Babu mimi nilikuwa kule maji yanakoelekea, wewe upo huku maji yanakotokea.” Staili ya kwanza ikafeli. Akatafuta ya pili: “Wewe unakumbuka mwaka uleee ulivyonitukana?” Mwana kondoo akashangaa tena: “Mimi nimezaliwa mwaka huu, hadi sasa nina miezi minne tu.” Mbwamwitu akaona akifanya mzaha ataukosa mnofu huu.
Akasema: “Basi kama si wewe alikuwa baba yako maana nilikutana naye hapa hapa!” Mwanakondoo akajibu: “Mama alikuja hapa kutokea ng’ambo akiwa mjamzito. Mimi sijapata kumfahamu baba yangu.” Mbwamwitu akasema “Ndiye huyohuyo! Kama si yeye basi ni mama yako ndiye aliyenitusi maana mmefanana hadi kwato!” Mwana kondoo alizidi kushangaa, “Mbona mama yangu ni mweusi?” Mbwamwitu kusikia hivyo alimfuata akiwa tayari kumdhuru: “Si nilisema? Watoto wa kizazi kipya hamna adabu... Unanitukana tena? Ngoja nikufunde...”
Lakini kwa bahati pale mtoni alikuwapo mbweha mzee. Akasema: “Unaweza kumla huyo mtoto lakini kamwe hutaijua Elimu yake. Lakini unaweza kutumia akili zake na ukapata mawindo yako kwa urahisi. Akili ni bora kuliko mabavu.” Mbwamwitu aliondoka kichwa chini huku akinong’ona: “Nilikuwa namtania tu...”
Nelson Mandela alifungwa gerezani miaka 27 mfululizo. Alikuwa na jeshi la wafuasi lililokuwa tayari kutoa maisha kwa ajili yake. Jeshi la Wazulu, Wakhosa na Wanandi lilipopanda mzuka lililizidi lile la Kimasai. Lakini Mandela alipata kusema: “Elimu ni silaha yenye nguvu unayoweza kuitumia kuibadilisha dunia.”
Yaani hata kama wangetumia nguvu wakati ule naye akaachwa huru, bado kungekuwa na uwezekano wa kuzidiwa akili na makaburu walionuia kumla mwanakondoo.
Patrice Lumumba katika barua yake ya mwisho kwa mkewe, Pauline aliandika: “Siku moja Historia itajieleza; haitakuwa Historia inayotolewa Umoja wa Mataifa, Washington, Paris wala Brussels, bali ni Historia ya Afrika. Siku moja Afrika itaandika Historia yake yenyewe, Kusini na Kaskazini mwa Jangwa la Sahara kutatukuka.”
Baadhi ya watu walipata shida na filosofia za wazee wetu. Tutawezaje kufanya haya wanayosema na tumezoea utwana? Kwame Nkurumah alijibu: “Njia nzuri ya kujifunza uhuru ni kuwa huru.” Alimaanisha ukitaka kujifunza kuishi, kwanza ishi.
Haile Selassie I Mfalme wa Ethiopia alisema: “Elimu inaendeleza uwezo wako wa kufikiri; na uwezo huo hukutofautisha wewe na viumbe wengine. Ni Elimu inayomwezesha mtu kuyatawala mazingira yake, kuyafanyia kazi na kutumia rasilimali iliyopo kwa usitawi wa maisha yake. Ufunguo wa maisha bora ni Elimu kwa kuwa mtu huyu hataishi kwa mkate pekee.”
Martin Luther King, mwanaharakati wa Kiafrika aliyeuawa Marekani aliiona Elimu kuwa nyenzo inayomwelekeza mtu kufikiri na kuishi kwa umakini: akili jumlisha tabia yake. Hilo ndilo alilolisema kuwa ni lengo la elimu ya kweli. Mwanaharakati mwingine Malcom X alisema Elimu ndiyo hati ya kusafiria kwenda kwenye wakati ujao, kwa kuwa kesho ipo kwa ajili ya wanaoiandaa kuanzia leo.
Tukubali ama kukataa, lakini ukweli utabaki kuwa kweli. Hapa haizungumziwi elimu ya propaganda, bali ni ile mtu anayozaliwa nayo na kuikuza. Hakuna kabila, dini wala taifa linalokataza mtu kuwa na elimu. Lakini kinachozuiwa ni aina ya elimu unayoichukua.

Wenzetu hadi leo wana matabaka. Zipo familia zilizotukuka na zipo familia dhalili. Sisi hatuna mambo hayo, ndiyo maana tulipotawaliwa na kujikomboa tuliamua kuyafuta yale tuliyoambukizwa. Lakini jini lililotolewa miilini mwetu haliwezi kuondoka kwa urahisi bila kwenda kuomba msaada kwa majini wenziwe.
Mwalimu Nyerere aliwafafanulia watu wake kwa hili: “Inawezekana tatizo la paka kwa panya lingekwisha kama paka angefungiwa kengele shingoni: tabu ni kumpata panya wa kuifanya kazi hiyo. Pia panya watakuwa wajinga sana wakidhani kuwa paka watajifunga au watafungana kengele shingoni.”
Ujinga ni adui mkubwa maendeleo. Unapofanya ujinga usidhani kuwa unaowafanyia ndiyo pekee watakaoathirika. Uelewe wazi kuwa hata wewe mwanzisha ujinga hutaendelea hata dunia iache kuzunguka.
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa