Home » » KIGOGO CHADEMA AVULIWA UONGOZI

KIGOGO CHADEMA AVULIWA UONGOZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Kanda ya Magharibi,kimemvua uongozi Katibu wa chama hicho Jimbo la Geita,Rogers Ruhega, huku kikitengua uamuzi wa kuwavua uanachama vigogo wake 10 waliotuhumiwa kwa usaliti.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu jana,Mwenyekiti wa Chama hicho Kanda ya Magharibi, Peter Mekele,alithibitisha kuvuliwa madaraka kwa kigogo huyo.

Alisema uamuzi huo ulifikiwa baada ya kuwepo mashauriano na uongozi wa chama ngazi ya taifa.

"Ni kweli tumemvua uongozi Katibu wetu wa Jimbo la Geita kutokana na matumizi mabaya ya madaraka,ambapo ameonekana kutumia cheo chake kuwakandamiza wagombea wenzake kwa kuwaita wasaliti... lakini pia kikao kilichofanya uamuzi wa kuwavua wanachama 10 akiwemo diwani viti maalum kata ya Kagu, Malcelina Simbasasa, hakikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo," alisema.

Alisema, tayari Rogers amekwishapokea barua hiyo ya kumvua uongozi. Alisema mbali ya uamuzi huo,pia chama hicho kimesema viongozi wote wa jimbo hilo hawaruhusiwi kujishughulisha na shughuli zozote za kiuongozi zinazohusiana na uchaguzi.

Chama hicho sasa kimemteua, Amos Nyanda, kuwa mratibu wa uchaguzi wa jimbo hilo.

Alisema wanachama wote waliokuwa wamevuliwa uanachama na Kamati tendaji ya jimbo iliyokutana juzi hivi sasa ni wanachama halali na wana sifa zote za kugombea nyadhifa mbalimbali ndani ya chama hicho.

Kutokana na uamuzi huo alisema uchaguzi katika jimbo la Geita,ambao umekuwa ukiahirishwa mara kwa mara sasa utafanyika Agosti 17, mwaka huu.

Juhudi za kumpata Rogers ili kuzungumzia hatua hiyo hazikuzaa matunda,baada ya simu yake ya mkononi kuwa haipatikani.

Hivi karibuni chama hicho kimekuwa katika hali ya migogoro ambapo baadhi ya wanachama na viongozi wake wamefikia hatua ya kutuhumiana kusaliti chama huku baadhi yao wakitajwa kuwa wafuasi wa aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Taifa, Zitto Kabwe.

Chanzo:Majira

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa