Home » » TAALUMA YA UALIMU YATOA NYOTA WENGI AFRIKA MASHARIKI

TAALUMA YA UALIMU YATOA NYOTA WENGI AFRIKA MASHARIKI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Eric Anthony
Mama Janet Magufuli, Mke wa Rais wa Tanzania, Dk John Pombe Magufuli.
NDIVYO wanavyotania, eti ukitaka kushika wadhifa mkubwa katika Serikali ya Kenya, basi oa mwalimu! Wanadai ndiyo `nyota’ mpya ya madaraka ilikolalia.
Kisa? Kwa kuwa Margaret Kenyatta, mke wa Rais Uhuru Kenyatta kitaaluma ni mwalimu, pia Rachel Ruto, mke wa Naibu Rais wa Kenya, William Ruto ni mwalimu. Ukiachilia mbali hao, hata Ida Odinga, mke wa Raila Odinga, Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya ambaye mara mbili amemtoa jasho Uhuru Kenyatta katika kuwania urais wa Kenya, naye ni mwalimu.
Margaret na Rachel walisomea ualimu katika Chuo Kikuu cha Kenyatta wakati Ida alisoma katika Chuo Kikuu cha Nairobi. Hata Lucy Kibaki, mke wa Rais wa Tatu wa Kenya, Mwai Kibaki naye alikuwa mwalimu kitaaluma.
Alifundisha katika Vyuo vya Ualimu Kamwenja na Kambui ambako alipanda na kuwa Mkuu wa Chuo. Hata hivyo, baada ya kuolewa na Kibaki mwaka 1961, alifanya kazi kwa miaka miwili tu na baadaye kuachana na taaluma hiyo.
Rais wa pili wa Kenya, Daniel Arap Moi ambaye wiki iliyopita, Agosti 22, alitimiza umri wa miaka 92, naye kitaaluma ni mwalimu. Mazingira ya Kenya yanaonekana kutotofautiana sana na Tanzania, kwani chati ya walimu katika kushika madaraka au kuwa wake wa viongozi wakuu imeonekana kuwa juu.
Kuanzia Mkuu wa nchi, Rais Dk John Magufuli na Mkewe, Mama Janeth Magufuli, kitaaluma ni walimu na wamefanya kazi ya ualimu. Vivyo hivyo kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ni mwalimu kitaaluma kama ilivyo kwa Mkewe, Mary Majaliwa.
Kwa Tanzania, Mama Magufuli si mke wa kwanza wa Rais kuwa mwenye taaluma ya ualimu, kwani hata Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, mkewe Mama Salma Kikwete ni mwalimu kitaaluma.
Pia, hao si wa kwanza, kwani mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mama Maria, naye kitaaluma ni mwalimu. Mama Maria aliyezaliwa mwaka 1930 akiitwa Maria Waningu Gabriel Magige, alisoma Shule ya Watawa Wakatoliki Nyegina, Musoma na Ukerewe mkoani Mwanza.
Baadaye alijiunga na Chuo cha Ualimu Sumve. Alifundisha shule ya Msingi Nyegina kabla ya kuolewa na Mwalimu Nyerere mwaka 1953. Aidha, Rais wa Awamu ya Pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi aliyezaliwa miaka 92 iliyopita, alianzia ajira yake kwa kushika chaki katika Shule ya Msingi Mangapwani ambako pia alisoma na kuhitimu elimu ya msingi.
Nchini Uganda, Rais wa nchi hiyo, Yoweri Museveni ingawa kitaaluma ni mchumi na aliyebobea katika Sayansi ya Siasa, amewahi kufundisha Chuo cha Ushirika Moshi, mkoani Kilimanjaro wakati Mkewe, Janeth Museveni, ni mwalimu kitaaluma aliyesomea katika Chuo Kikuu cha Makerere. Kwa sasa ndiye Waziri wa Elimu na Michezo wa Uganda.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa