Home » » Utalii wa kiutamaduni unakuza uchumi binafsi

Utalii wa kiutamaduni unakuza uchumi binafsi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Utalii wa kiutamaduni bado ni nadharia changa katika nchi za ulimwengu wa tatu ikiwemo Tanzania,kwa kuwa nchi hizo zimezoea kuona utalii wa asili wa kutembelea mbuga za wanyama.
Siku za nyuma vivutio vya utalii wa kiutamduni kama vile majengo ya kale,maeneo ya kihistoria na makumbusho hayakupewa mtazamo wa kiuchumi zaidi.
Maeneo hayo yalipewa mtazamo wa kielimu zaidi na kuundwa Idara ya Mambo ya Kale na Idara ya Makumbusho ambazo zote awali zilikuwa katika wizara ya elimu na utamaduni ambavyo viliwekwa kama vyanzo vya elimu zaidi kuliko vyanzo vya utalii.
Mabadiliko katika ulimwengu mzima ndiyo yaliyosukuma kuwepo kwa utalii wa kiutamduni na nchi zilianza kutoa kipaumbele katika utalii wa kiutamaduni ndiyo maana hapa nchini idara za mambo ya kale na makumbusho zilihamishwa kutoka Wizara ya Elimu na kuingia Wizara ya Utalii na Maliasili.
Hata hivyo ni vigumu kutenganisha utalii asili na utalii wa kiutamduni kutokana na aina hizo mbili za utalii kuwa na mahusiano ya karibu,Mtalii anapokwenda kutembelea utalii wa asili kama mbuga za wanyama pia anaweza kupita katika maeneo yenye utalii wa kiutamaduni na kununua bidhaa mbalimbali za kiutamaduni.
Wananchi, katika utalii wa utamaduni, wanaweza kunufaika kuanzia kiwango cha familia, mtaa, kitongoji, kijiji, wilaya, mkoa na kitaifa kwa hiyo utalii wa kiutamaduni unatoa fursa kubwa ya ukuaji wa uchumi kuanzia kwa mtu binafsi hadi kwa taifa.Utafiti umebaini kuwa utalii wa kiutamaduni unaweza kubadilisha kiwango cha maisha ya watu kutokana na kupata kipato kinachoweza kuwaongezea kipato cha ziada katika mapato yao.
Kwa mfano kabila la wamasai katika msimu wa utalii wa kiutamaduni wanapata mapato karibu shilingi 30,000 kwa siku kutokana na aina hiyo ya utalii.
Utafiti umebaini kuwa kofia inayotengenezwa kwa ukindu inauzwa kati ya Sh3,500 hadi 5,000, mkanda unaotengenezwa kwa ngozi yenye shanga unauzwa kati ya Sh5,000 hadi 10,000 na kinyago cha kuchongwa kinauzwa kuanzia Sh20,000 hadi 500,000 kutegemea na ukubwa wa kinyago hicho.
Utalii wa kiutamaduni una nafasi kubwa ya kuchangia uchumi wa watu binafsi kwa sababu utalii unatengeneza ajira za moja kwa moja na ajira ambazo sio za moja kwa moja na hivi sasa Watanzania wengi wamejiajiri katika shughuli za utalii wa kiutamduni kwa kufungua maduka ambayo wanauza vitu vya kitamaduni vyenye bei kubwa zaidi katika soko la utalii.
Watu wanaonufaika katika sekta ya utalii wa kiutamduni kutoka katika migongo ya watu wengine ni pamoja na watu wenye hoteli, nyumba za kulala wageni, watu wanaouza maji na vyakula mbalimbali.
Hivi sasa kuna nchi nyingi ambazo zimekuza uchumi wake kwa haraka kupitia utalii wa kiutamaduni zikiwemo Australia, Ujerumani, Uingereza pamoja na nchi nyingine nyingi za ulaya ambazo kutokana na ukosefu wa mbuga za wanyama zimeamua kuendeleza utalii wa kiutamaduni zaidi kuliko utalii wa asili na kupata maendeleo makubwa kupitia aina hiyo ya utalii.
Sekta ya utalii nchini ni mhimili wa maendeleo ya uchumi kwa kuwa ina mchango mkubwa katika pato la Taifa kwa kuchangia wastani wa asilimia 17.
 
Endapo Sekta hii itasimamiwa vizuri na uendelea kupewa kipaumbele na Serikali ni dhahiri kwamba uchumi wa Taifa utaimarika na kupunguza tatizo la umaskini nchini.
Albano Midelo ni mwandishi mwandamizi anayeandikia masuala ya maendeleo,madini,mafuta na gesi
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa