Home » » WANANCHI GEITA WAOMBA MKOA WA KIPOLISI ILI KUTHIBITI UHALIFU

WANANCHI GEITA WAOMBA MKOA WA KIPOLISI ILI KUTHIBITI UHALIFU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 NA,MWANDISHI WETU GEITA

Jitihada za jeshi la Polisi mkoani Geita,kuimarisha ulinzi ukiwemo ulinzi shirikishi jamii zimezidi kugonga mwamba,kutokana na mkoa huo kuzidi kukumbwa na matukio ya uharifu kama ujambazi,mauaji ya vikongwe na ubakaji.

Kushindwa kufanikiwa kwa ulinzi huo ni kutokana na mfululizo wa matukio 8 yaliyotokea katika kipindi kisichozidi mwezi mmoja yakifuatiwa na tukio lililotokea jana,Mtaa wa Shilabela kata ya Kalangalala mjini Geita baada ya mlinzi wa Vibanda vya Biashara Juma Suguta(40) kuuawa na watu wasiojulikana.

Mlinzi huyo ambaye ni mkazi wa Mtaa jirani wa Moringe mjini hapa,aliuawa usiku wa kumkia jana kwa kuchinjwa shingo kisha wauaji kufungua kibanda kimoja wapo cha Mwalimu Jackson Mayunga wa shule ya Gold Valley ingawa hawakuchukua kitu chochote.

Kamanda wa polisi mkoani Geita,Joseph Konyo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa juhudi za kuwasaka wauaji hao zinaendelea.

‘’Tukio lipo na OCD(Mkuu wa Polisi wilaya),na OC-CID(Mkuu wa Upelelezi),nimewapa maelekezo ya kuhakikisha  wahusika wa mauaji hayo wanatiwa mbaroni’’alisema Kamanda Konyo.

Aidha taarifa kutoka eneo la tukio hilo zilizothibitishwa na ofisa mtendaji wa kata ya Kalangalala,Hamad Husein aliyefika eneo hilo mapema ni kwamba mlinzi huyo amekutwa amekufa huku akiwa amelazwa kifudifudi na walipomgeuza alionekana akiwa amechinjwa shingo huku akiwa amepingwa kitu kizito kichwani.

‘’Huyu mlinzi nilikuwa namfahamu sana,ni rafiki yangu wa karibu taarifa zake nimezipata asubuhi ya saa 12 nilipigiwa simu lakini nilipofika eneo la tukio nimeona damu nyingi zikiwa zimetapakaa,Tulipomgeuza alikuwa amechinjwa shingo na kwamba wauaji hawakuchukua kitu chochote’’alisema Mtendaji Hamad.

Tukio hilo ni la pili kutokea katika kipindi kisichozidi mwezi mmoja baada mlinzi wa Kampuni ya ulinzi ya Geita(GSG),Kulwa Kanuka(38)kuuawa kikatili Aprili 4,mwaka huu kwa kuchinjwa shingo na watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi kisha kumnyofoa sehemu zake za siri na kumtoboa macho.

Mlinzi huyo aliuawa akiwa lindoni mtaa wa Mbugani na kwamba wauaji walivunja kibanda cha M-pesa na kuchukua sh.45,000 pamoja na viti vine vya Plastiki.

Mbali na tukio hilo mkoa wa Geita umezidi kukumbwa na matukio ya mauaji ya vikongwe ambapo katika kipindi hicho vikongwe wane wameuawa na majina ya vijiji katika mabano  ni Kulwa Kapalata(67)(Katoma),Joyce Dotto(70)(Butundwe)Yombo Petrol(50)(Kanyala),na Kabula Yohana(60)(Kagu).

Hata hivyo matukio hayo yamefuatiwa na tukio la kusikitisha lililotokea Mei 2,mwaka huu,baada ya mwanafunzi wa darasa la pili shule ya msingi Kalangalala mjini Geita,kubakwa hadi kufa na mtu alimvamia ndani akiwa amelala huku mama yake mzazi akiwa kazini kwenye uhudumu wa baa.

Kufuati kuwepo kwa mfululizo wa matukio hayo wakazi wa mji wa Geita wameomba mkoa huo kuwa na kanda maalumu ya kipolisi ili kuthibiti uharifu ambao umeleta hofu kwa wakazi hao.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa