Home » » WAFUNGA OFISI YA SERIKALI KWA UHARIBIFU

WAFUNGA OFISI YA SERIKALI KWA UHARIBIFU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
TUHUMA za ubadhirifu na uporaji wa ardhi zinazowakabili baadhi ya watendaji wa halmashauri na kijiji, zimewasukuma wananchi wa Kijiji cha Bugulula, Kata ya Bugulula wilayani Geita kufunga ofisi ya serikali ya kijiji hicho.
Baadhi ya tuhuma zilizowafanya wanakijiji hao kufunga ofisi yao ni pamoja na ujenzi mbovu wa msingi wa zahanati ya huduma ya mama na mtoto uliogharimu kiasi cha sh milioni 36, wakati tayari ukiwa umeweka nyufa.
Wananchi hao zaidi ya 250 walisema viongozi wa serikali ya kijiji hicho wameshirikiana na baadhi ya watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita kuhujumu kiasi hicho cha fedha kwa kumpa kazi ya ujenzi wa jengo hilo mkandarasi ambaye ujenzi wake uko chini ya kiwango.
Mmoja wa wananchi hao aliyeomba jina lake lihifadhiwe, alisema ujenzi mbovu wa msingi wa jengo hilo ni aina nyingine ya kielelezo cha kukithiri kwa ufisadi unaofanywa na baadhi ya watendaji wa serikali na halmashauri ya wilaya hiyo.
Mmoja wa kina mama wa kijiji hicho ambaye pia aliomba jina lake lisitajwe gazetini, akizungumza kwa uchungu alisema: “Tunapata shida sana kina mama wakati wa kujifungua, ukipatwa na uchungu inabidi uende Geita ambako ni mbali,  hivyo tulijua jingo hilo ndiyo mkombozi wetu.”
Hata hivyo, viongozi na watendaji kadhaa wa serikali ya kijiji na halmashauri wametupiana mpira, kila mmoja akielekeza lawama kwa mwingine.
Wakati Diwani wa Kata hiyo, Elisha Lupuga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Halmahauri ya Wilaya ya Geita akipuuza malalamiko ya wananchi hao na kudai kuwa hakuna malalamiko yoyote ya msingi, bali kundi la vijana vijana wachache waliopandikizwa kufanya fujo katika kijiji hiki, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji, Bahati Matitu, alikiri ujenzi duni wa msingi wa jengo.
“Ni kweli msingi una ufa na tayari mkandarasi tulimwambia na anakuja kuurekebisha ili atukabidhi,” alisema Matiku.
Hata hivyo, taarifa ya halmashauri iliyosomwa katika kikao cha baraza la madiwani mapema mwaka huu, imeonyesha kuwa ujenzi wa msingi huo umekamilika kwa asilimia mia moja na tayari umekabidhiwa.
Mkandarasi aliyejenga msingi huo, Kenedy  Kubuka kutoka Kampuni ya J.V.K  alipoulizwa kuhusiana na tuhuma hizo, alikiri kuwepo na dosari katika ujenzi.
“Ni kweli sisi ndio tunajenga jingo hilo, lakini ujenzi unaendelea na bado sijamaliza na kuanzia wiki ijayo nitakamilisha pale palipobaki na ndiyo maana sijakabidhi rasmi,” alisema Kubuka.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Ali Kidwaka alipohojiwa sababu za kulipwa kwa fedha hizo wakati ujenzi umefanyika chini ya kiwango, alijibu kwa kifupi: “Sijui kama kuna msingi unajengwa katika kijiji hicho na kama upo nitafuatilia ili nijue zaidi.”’
Hata hivyo, uchunguzi umebaini kwamba mkandarasi huyo amelipwa tu nusu ya sh mil 36.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa