Home » » Auawa akidaiwa kuiba mahindi mabichi

Auawa akidaiwa kuiba mahindi mabichi

Geita. Mwanamke aliyefahamika kwa jina la Sambila Mihayo anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 20 hadi 22 ameuawa kinyama na wananchi wenye hasira baada ya kukamatwa akiiba mahindi mabichi shambani katika Kitongoji cha Ilolanguli Kijiji cha Mbabani Wilaya ya Geita mkoani hapa.
Tukio hilo lilitokea jana saa 9:00 usiku ikiwa ni siku moja baada ya sherehe za kuanza kwa mwaka mpya 2014.
Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Abel Kidesheni alisema alisikia mayowe ya wananchi na alipofika eneo la tukio alikuta tayari mwanamke huyo akiwa ameuawa na wananchi hao huku mwili wake wakitaka kuuteketeza kwa moto.
Kidesheni alisema mwanamke huyo alikutwa akikata mahindi kisha kuyapakia kwenye mfuko wa sandarusi ndipo alipokamatwa na wananchi ambao walimshambulia kwa mawe, marungu na fimbo hadi kupoteza maisha yake.
Kamanda wa Polisi mkoani Geita, Leonard Paulo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kudai kwamba uchunguzi unaendelea ikiwa ni pamoja na kuwabaini wote waliohusika na kwamba hakuna mtu aliyeshikiliwa kuhusiana na tukio hilo.
Akizungumza na gazeti hili, mke wa mmiliki wa shamba hilo Milika Migeka (41) alisema wakiwa wamelala walisikia mtu akivunja mahindi awali walifikiri ng’ombe ndipo walipotoka taratibu na kumkuta mwanamke huyo akiendelea kukata mahindi shambani mwao.
Alisema baada ya kuona hali hiyo walipiga mayowe ambayo yaliwaamsha majirani.
‘’Baada ya majirani hao kufika walianza kumpiga kwa fimbo,mawe na marungu hadi kumuua na baadaye walitaka kumchoma moto lakini mwenyekiti aliwazuia,’’alisema Migeka.
Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho Petro Manyama alidai kusikitishwa na uamuzi uliochukuliwa na wananchi hao na kukemea vikali vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mikononi.
Tukio hilo ni pili kutokea mkoani Geita katika kipindi kisichozidi wiki moja baada ya wanaume watano kuuawa kwa kukatwa kwa mapanga kisha miili yao kutoeketezwa kwa moto baada ya kuiba rambi rambi msibani kitongoji cha Nyantorotoro A,mjini Geita.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa