Home » » Mwandishi Mwananchi ajeruhiwa mikononi mwa polisi

Mwandishi Mwananchi ajeruhiwa mikononi mwa polisi

Geita.Mwandishi wa habari wa Magazeti ya Mwananchi Communications Ltd, mkoani Geita, Salum Maige amejeruhiwa vibaya jichoni baada ya kushambuliwa na kundi la watu wanaodaiwa kuwa ni askari wa Kituo cha Polisi Geita.
Akizungumza jana akiwa katika Hospitali ya Geita alikokuwa amelazwa, Maige alisema alikumbwa na mkasa huo wiki iliyopita.
Alidai kuwa alivamiwa na kundi la askari polisi zaidi ya wanane Ijumaa iliyopita ambao walimpiga na kumjeruhi vibaya kiasi cha kulazwa kwa siku mbili katika hospitali hiyo kabla ya kuruhusiwa.
Alisema tukio la kupigwa kwake lilitokea mita 60 kutoka zilipo Ofisi za Polisi Mkoa wa Geita pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Pudensiana Protas alithibitisha kupewa taarifa juu ya kukamatwa kwa mwandishi huyo lakini hakujulishwa juu ya kupigwa na kujeruhiwa. Hata hivyo, baada ya kuonyeshwa picha za mwandishi huyo zikionyesha alivyojeruhiwa, aliahidi kumtafuta ili kujua undani wa tukio hilo.
Akisimulia mkasa huo, alisema siku hiyo akiwa anapita katika Mtaa wa Bomani kuelekea nyumbani kwake, alikutana na kundi la askari polisi waliokuwa kwenye gari la jeshi hilo ambao baada ya kumwona, alidai kuwa baadhi yao walishuka na kumfuata huku wakitoa amri ya kusimama na kwamba yupo chini ya ulinzi.
Alisema aliwauliza sababu za kuwekwa chini ya ulinzi lakini badala ya kumjibu walimshika na kumfunga pingu mikononi kisha kumtupa ndani ya gari lao.
Alisema akiwa ndani ya gari hilo walianza kumshambulia kwa kumpiga na kumsababishia maumivu makali sehemu mbalimbali za mwili.
Katika kipigo hicho, alisema alipoteza kamera aina ya Canon yenye thamani ya Sh350,000, kifaa cha kurekodia sauti chenye thamani ya Sh150,000, kitambulisho cha kazi na fedha taslimu Sh16,000.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa