DC MASALLA ASHAURI MAONESHO YA NANENANE YAVUTIE ENEO LA MAZIWA MAKUU

Waandaaji wa maonesho ya Nanenane mikoa ya Kanda ya Ziwa Magharibi Mwanza,Geita na Kagera wameshauriwa kuzidi kuipa hamasha maonesho hayo na kuzifikia nchi zote za maziwa makuu kutokana na Mkoa wa Mwanza kuwa eneo la kimkakati.

Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mhe.Hassan Masalla alipotembelea baadhi ya mabanda na kujionea na kupata taarifa mbalimbali kutoka kwa washiriki na kuhimiza fursa ya Mwanza kuwa eneo la kimkakati itumike vizuri kuyapa wigo maonesho hayo.

"Mwanza siku chache zijazo itazidi kuimarika hasa katika eneo la usafiri kuanzia wa anga,reli na barabara hivyo ni wakati mwafaka kwa waandaaji kuja na ubunifu wenye sura ya kimataifa utakao leta tija ya kiuchumi.

Amesema ukanda huu wa nchi za maziwa makuu umejaa wakulima na wafugaji,na makundi mengine na katika maonesho haya kuna utoaji wa elimu ya kitaalamu namna ya kupata tija hata ukiwa na mifugo michache au kuvuna mazao bora kwa muda mfupi bila kitegemea mvua.

Aidha Mkuu huyo wa Wilaya amewataka Taasisi mbalimbali zinazotoa huduma za Utafiti wa kilimo kwa ujumla ziongeze huduma hizo kwa wakulima wote nchini kutokana na sekta hiyo kuingiza fedha nyingi hivi sasa.

Viongozi mbalimbali wanaendelea kuyatembelea maonesho hayo yatakayo fikia tamati Agosti 8 mwaka huu.

Kauli mbiu ya maonesho hayo ni”chagua viongozi bora wa Serikali za mitaa kwa maendeleo endelevu ya kilimo,mifugo na uvuvi.”

 


RAS GEITA AYAZINDUA RASMI MAONESHO YA NANENANE KANDA YA ZIWA MAGHARIBI.

Maonesho ya Nanenane 2024 Kanda ya Ziwa Magharibi yamezinduliwa rasmi leo Agosti 3,2024 kwenye viwanja vya Nyamhongolo huku yakionesha kuzidi kupata hamasa kutoka kwa wananchi.

Akifungua maonesho hayo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita,Katibu Tawala wa mkoa huo Mohamed Gombati amesema Jukwaa hilo liendelee kuwa somo kwa makundi mbalimbali yanayolengwa na maonesho hayo.

Akiwa na mwenyeji wake Katibu Tawala wa mkoa wa Mwanza Bw.Balandya Elikana,Gombati amatembelea mabanda mbalimbali na kujionea huduma zitolewazo na Taasisi,Halmashauri na makundi mbalimbali.

"Serikali ya Rais Samia ni kutaka Taifa lijitosheleze kwa chakula,uwekezaji katika kilimo na maendeleo ya viwanda, nimeona fursa hizo kutokea hapa Nanenane,"amesisitiza Gombati

Akitoa taarifa ya maonesho hayo Bw.Balandya amebainisha yamekuwa na tija kwa wajasiriamali kutokana na kupata elimu ya utaalamu namna ya kuendesha shughuli zao.

"Eneo letu idadi kubwa ni wafugaji na wavuvi,Serikali inaendelea kuwekeza katika sekta hii hivyo wakulima wanafaidika kwa kufanya shughuli zao kwa tija",Balandya.

Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Emil Kasagara amebainisha maonesho ya mwaka huu hadi siku ya jana walikuwa na washiriki zaidi ya 5,000 wakitoa huduma mbalimbali.

Maonesho hayo yatafikia kilele Agosti 8 mwaka huu na mgeni rasmi atakuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe.Said Mtanda

 

VICTORIOUS CENTRE CENTER OF EXCELLENCY WAWEKA MIKAKATI KUWASAIDIA WENYE USONJI


Na Mwandishi Wetu

KITUO cha Victorious Centre of Excellency nchini Tanzania kimesisitiza dhamira yake ya kujitolea katika kutoa matibabu ya uhuishaji na elimu kwa jamii kuhusu mahitaji maalumu kwa watoto wenye hali ya usonji hapa nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Victorious Centre of Excellency, Sarah Laiser-Sumaye ameelezea dhamira ya kituo hicho jijini Dar es Salaam hivi karibuni kwenye Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Nelson Mandela yaliyoratibiwa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Ubalozi wa Afrika Kusini nchini na kituo cha Victorious Centre of Excellence.

Kupitia maadhimisho hayo wadau hao walifanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo upandaji miti, kutoa misaada mbalimbali, kupaka rangi kuta na kusaidia kazi za jikoni kwenye kituo hicho, ikiashiria juhudi zao za pamoja katika kuimarisha maisha ya watoto wenye mahitaji maalumu.

Akizungumza kwenye tukio hilo, Sarah Laiser-Sumaye alisema ongezeko la kesi za hali ya usonji nchini Tanzania na nchi za Afrika kwa ujumla ni jambo la kuchukua hatua mapema, huku utafiti wa hivi karibuni kutoka kituo cha Kudhibiti Magonjwa (CDC) cha nchini Marekani ukibainisha kuwa mtoto mmoja  kati ya watoto 36 wanakabiliwa na changamoto ya hali ya Usonji.

"Watoto wenye hali ya Usonji hukumbana na changamoto katika mawasiliano, kushindwa kutamka maneno vizuri, hukabiliwa na ugumu katika kupokea mafunzo ya kielimu na mara nyingi huonyesha tabia za ukorofi kupindukia," Sarah Laiser-Sumaye alieleza.

 "Changamoto hizi huongezeka zaidi kutokana na uelewa hafifu na imani za kiutamaduni zinazohusiana na changamoto ya Usonji katika ukanda wa Africa,’’.

Hata hivyo, alibainisha kuwa Kituo cha Victorious Centre of Excellency na Victorious Academy vimeibuka kama alama ya matumaini na usaidizi kwa watoto wenye changamoto hiyo na familia zao. 

Kupitia matibabu yao ya uhuishaji na elimu ya mahitaji maalumu, vituo hivyo vinapambana kuleta tofauti inayokusudiwa katika maisha ya watoto hao wenye mahitaji maalumu pamoja na familia zao.

Kituo hicho kinatoa huduma mbalimbali za tiba ya urekebishaji (rehabilitation therapies) na shughuli za ziada kwa watoto wenye hali ya usonji nchini Tanzania kwa lengo la kuwajumuisha katika jamii kupitia juhudi makini za kujengea uelewa wa kijamii.

Katika kuthibitisha uzito na umuhimu wake, tukio hilo lilipambwa na uwepo wa wadau muhimu kutoka taasisi hizo akiwemo Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania, Noluthando Mayende-Malepe, Mkuu wa Ofisi ya Msimamizi Mkazi wa UN, Shabnam Mallick, Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Frederick Sumaye.

Wengine ni  Waziri Mstaafu wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula, Balozi wa Umoja wa Comoro na Mkuu wa Msafara wa Kidipromasia, Dk. Ahamada El Badaoui Mohamed Fakih pamoja na Mabalozi wengine kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Congo, Algeria, Namibia, Msumbiji na wengine wengi.
 
Balozi Mayende-Malepe, akizungumza kwenye tukio hilo alionyesha kutambua umuhimu wa kazi zinazofanywa na Kituo cha Victorious Centre of Excellency huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano na taasisi kama hiyo ili kuinua ufahamu na kupanua muelekeo wa fikra, mtazamo na maadili ya Hayati Mandela, ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya uonevu na kusaidia watu wenye uhitaji.

"Siku ya Kimataifa ya Nelson Mandela ni fursa kwa wananchi duniani kote kwa kutambua nguvu zao binafsi za kubadili dunia kuwa sehemu nzuri na njema ya kuishi.Kupitia ushirikiano na taasisi kama Kituo cha Victorious Centre of Excellency, tunatambua pia tunaweza kuwa sehemu ya kuinua ufahamu na kupanua muelekeo wa maadili na fikra za Mandela ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya ukatili na kusaidia watu wenye uhitaji maalum," Alisema Balozi Mayende-Malepe

Umoja wa Mataifa pia ulionyesha kuguswa kwake na jitihada za Kituo cha Victorious Centre of Excellency huku ukionyesha kutambua umuhimu wa uongozi wa Nelson Mandela na umuhimu wa kukuza maadili yake na kuhamasisha watu kuwa na mchango chanya kwa jamii.

"Kila kitendo uhesabiwa hata kikiwa kidogo. Iwe ni kuchora ukuta au kusaidia kuandaa chakula, michango yetu leo ni sehemu ya jitihada kubwa ya kimataifa ya kupambana na umaskini na ukosefu wa usawa. Vitendo hivi vya huduma hata kikiwa ni kidogo athari zake chanya huenea nje kwa ukubwa zaidi.’’ Alibainisha Bi. Shabnam Mallick, Mkuu wa Ofisi ya Msimamizi Mkazi wa UN nchini Tanzania.

Hatua ya wadau hao ilikuja huku Kituo cha Victorious Centre of Excellency kikiwa kinaendela kujipambanua kama mdau muhimu sio tu katika kutoa huduma zake, bali pia kuwezesha jamii, kukuza ufahamu na kuunda jamii inayowajibika. 

Kupitia juhudi zake endelevu kituo hicho si tu kinabadilisha maisha ya watoto wenye hali ya usonji, bali pia kinawajuza wengine kufuata nyayo za Hayati Nelson Mandela, kufungamanisha dhana ya ‘Ubuntu’ (Utu) na kutimiza wajibu wake kwa kuzingatia mustakabali bora kwa wote.
Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Frederick Sumaye (wa pili kushoto) akizungumza na washiriki wakiwemo Mabalozi wa mataifa mbalimbali nchini Tanzania, pamoja na wakurugenzi wa mashirika katika maadhimisho ya Kimataifa ya Nelson Mandela yaliyoratibiwa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Ubalozi wa Afrika Kusini hapa nchini na kituo cha Victorious Centre of Excellency. Kupitia maadhimisho hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni, wadau hao walifanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kituo hicho ikiwemo upandaji miti, utoaji wa misaada ya kijamii, kupaka rangi kuta na kusaidia kazi za jikoni, ikiashiria juhudi zao za pamoja katika kuimarisha maisha ya watoto wenye mahitaji maalumu nchini. Wanaomsikiliza ni Waanzilishi na Wakurugenzi wa kituo hicho akiwemo Bw Filbert Sumaye (Kushoto) na Bi Sarah Laiser-Sumaye (wa pili kulia) pamoja na Mchungaji Dk. Eliona Kimaro (kulia)
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Victorious Centre of Excellency, Sarah Laiser-Sumaye akizungumza na washiriki wakiwemo Mabalozi wa mataifa mbalimbali nchini Tanzania, pamoja na wakurugenzi wa mashirika katika maadhimisho ya Kimataifa ya Nelson Mandela yaliyoratibiwa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Ubalozi wa Afrika Kusini hapa nchini na kituo cha Victorious Centre of Excellency. Kupitia maadhimisho hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni, wadau hao walifanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kituo hicho ikiwemo upandaji miti, utoaji wa misaada ya kijamii, kupaka rangi kuta na kusaidia kazi za jikoni, ikiashiria juhudi zao za pamoja katika kuimarisha maisha ya watoto wenye mahitaji maalumu nchini.

WANAFUNZI NAMNA PEKEE YA KUMLIPA RAIS SAMIA NI KUSOMA KWA BIDII-KATIMBA


Na Angela Msimbira, GEITA

NAIBU WAZIRI Ofisi ya Rais TAMISEMI (Elimu), Mhe. Zainab Katimba ametoa rai kwa wanafunzi wote nchini kuhakikisha wanasoma kwa bidii na kufaulu kwa viwango vya juu ili badae walitumikie taifa.

Mhe.Katimba ametoa rai hiyo alipotembelea shule mpya maalum ya wasichana ya sayansi ya Mkoa wa Geita kwa lengo la kukagua miundombinu iliyojengwa na kujionea maboresho yaliyofanywa na serikali katika ujifunzaji na ufundishaji kwenye sekta ya elimu nchini.

Amesema kuwa dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha watanzania wanapata elimu iliyobora katika mazingira mazuri hivyo ni wajibu wa wanafunzi kusoma kwa bidii ili kutimiza malengo yao.

“Namna pekee ya kumlipa Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha na kujenga miundombinu iliyobora na kuhakikisha mnapata elimu bila ada ni kuhakikisha na ninyi mnasoma kwa bidii, mfaulu vizuri na kupata elimu bora ili baadaye muweze kulitumikia taifa.”

Katimba amesema wanafunzi wanapaswa kutambua kuwa Taifa linawategemea, hivyo amewataka kuhakikisha hawafanyi mchezo wakiwa shuleni bali watumie fursa hiyo kujenga kesho yao.

Akitoa taarifa ya elimu Mkoa wa Geita, Katibu Tawala Mkoa huo, Mohamed Gombati amesema kwa upande wa shule ya sekondari ya wasichana imepokea Sh bilioni 3 katika awamu ya kwanza na Juni mwaka huu zimepokelewa Sh bilioni 1.1 kwa ajili ya kukamilisha baadhi ya majengo na tayari imeshaanza kuchukua wanafunzi.

Amesema kwa mwaka 2021/22 Mkoa wa Geita ilipokea Sh bilioni 17, mwaka 2022/23 zilipokelewa Sh bilioni 31 na kwa mwaka 2023/24 zilipokelewa Sh bilioni 32 bila kujumuisha fedha zinazotolewa kugharamia elimu bila ada.

Amesema kuwa katika fedha za ndani zinazoelekezwa kwenye miradi ya maendeleo za asilimia 60 au 40 kiwango kikubwa kinaelekezwa kwenye sekta ya elimu.

Awali, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya wasichana ya sayansi ya Mkoa wa Geita, Mwamin Kagoma amesema shule hiyo imegharimu Sh bilioni 4 na mpaka sasa wanafunzi 172 kati ya 211 waliopangiwa kujiunga na kidato cha tano wameripoti shuleni.







Wanaojiandikisha kuwa wapiga kura zaidi ya mara moja kutumikia kifungo jela

Na. Mwandishi Wetu, Geita

Wananchi watakaofanya udandanyifu ili wajiandikishe zaidi ya mara moja wanatenda kosa na wakibainika wanaweza kufungwa jela kifungo kisichopungua miezi sita na kulipa faini.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji (Rufaa) Jacobs Mwambegele leo tarehe 25 Julai, 2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani Geita.  

“Ningependa kusisitiza kuhusu suala la kujiandikisha kuwa mpiga kura zaidi ya mara moja, jambo hili ni kosa la kisheria kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 114(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na.1 ya Mwaka 2024,” amesema.

Jaji Mwambegele amefafanua kuwa kifungu hicho kinasema mtu yeyote atakayeomba kuandikishwa zaidi ya mara moja atakuwa ametenda kosa la kisheria na akitiwa hatiani adhabu yake ni faini isiyopungua kiasi cha shilingi laki moja (100,000/=) na isiyozidi shilingi laki tatu (300,000/=) au kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua miezi sita na kisichozidi miaka miwili au vyote kwa pamoja.  

Katika hatua nyingine, Jaji Mwambegele amesisitiza kuwa hakuna uwezekano wa mtu kujiandikisha  mara mbili na taarifa zake kusalia kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa kuwa kabla ya kutoa nakala ya mwisho, Tume hulisafisha Daftari kwa kuwaondoa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja.

“Mara baada ya uandikishwaji wa wapiga kura kukamilishwa, taarifa zote huingizwa kwenye mfumo wa AFIS (Automated Finger Print Identification System) ambao huwaonesha wote waliojiandikisha kwenye Daftari zaidi ya mara moja. Wapiga kura wa aina hii hufutwa moja kwa moja kwenye vituo vyote na kuwabakisha kwenye kituo alichojiandisha mara ya mwisho,” amesema.

Ameongeza kuwa orodha ya waliojiandikisha zaidi ya mara moja hupelekwa Jeshi la Polisi kwa ajili ya hatua za kisheria na kwamba Tume imefanya hivyo katika chaguzi za nyuma ambapo katika uandikishaji uliofanyika mwaka 2015, Tume ilibaini jumla ya wapiga kura 52,078 waliojiandikisha zaidi ya mara moja ambapo orodha yao ilikabidhiwa kwa Jeshi la Polisi tarehe 27 Agosti, 2015 kwa ajili ya hatua za kisheria.

“Katika uboreshaji wa Daftari wa mwaka 2020, Tume ilibaini majina ya watu 42,301 ambao walijiandikisha zaidi ya mara moja na orodha hiyo ilikabidhiwa kwa vyombo vinavyohusika na makosa ya kijinai,” amesema Jaji Mwambegele.

Ameeleza kuwa baada ya kukamilika kwa uchakataji wa Daftari, Tume huchapisha na kuweka wazi Daftari hilo chini ya kifungu cha 24 cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, Na. 1 ya mwaka 2024 ambapo wananchi hulikagua.

“Baada ya kukamilika kwa uchapishaji wa mwisho wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, vyama vya siasa hupewa nakala tepe (soft copy), haijawahi kutokea jina likajitokeza zaidi ya mara moja. Hivyo, hakuna uwezekano wa mtu kuandikishwa zaidi ya mara moja na kuweza kutumia nafasi hiyo kuwa kwenye vituo zaidi ya kimoja siku ya kupiga kura,” amesema Jaji Mwambegele.


 

MKUU WA MKOA GEITA AWATAKA WANANCHI KUJITOKEZA KWA WINGI KWENYE KAMPENI YA ELIMU KWA MLIPAKODI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 

MHE BITEKO AANZA KUTEKELEZA AGIZO LA WAZIRI MKUU LA KUKOMESHA UTORO MASHULENI, ACHANGIA MATOFALI 10,000 UJENZI WA MAABARA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akikagua majengo ya maabara za shule ya sekondari ya Kata ya Busonzo katika Kijiji cha Nampalahala akiwa katika ziara ya siku moja Wilayani Bukombe, Leo 2 Aprili 2018. Picha Na Mathias Canal-Wazo Huru Blog
Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akikagua nyumba ya walimu katika shule ya sekondari ya Kata ya Busonzo katika Kijiji cha Nampalahala, Leo 2 Aprili 2018. 
Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Nampalahala, Kata ya Busonzo wakifatilia mkutano wa hadhara ukiongozwa na Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko wakati akiwa katika ziara ya siku moja Wilayani Bukombe, Leo 2 Aprili 2018.
Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akizungumza na wananchi katika Kijiji cha Nampalahala, Kata ya Busonzo wakati akiwa katika ziara ya siku moja Wilayani Bukombe, Leo 2 Aprili 2018.
Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akikagua ujenzi wa nyumba za madaktari wa kituo cha afya cha Uyovu akiwa katika ziara ya siku moja Wilayani Bukombe, Leo 2 Aprili 2018.

Na Mathias Canal, Geita

Mbunge wa Jimbo la Bukombe Mkoani Geita ambaye ni Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko Leo 2 Aprili 2018 amechangia matofali 10,000  kwa ajili ya ukamilishaji Wa vyumba vya maabara ili kurahisisha uanzisha Wa shule ya sekondari Kata ya Busonzo Wilayani Bukombe.

Shule ya sekondari Busonzo inahitaji kukamilisha maabara tatu ili iweze kufunguliwa ambapo serikali imetoa milioni 40 kwa ajili ya kazi hiyo.

Mhe Biteko amechangia matofali hayo Mara baada ya maagizo ya Waziri Mkuu Mhe Kassim Majaliwa aliyoyatoa wakati Wa dhifa ya uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2018 katika uwanja wa Magogo mkoani Geita kwa kuwataka viongozi wa mikoa ya Tabora, Geita, Mtwara na Shinyanga ambayo inaongoza kwa utoro wa wanafunzi kwa shule za msingi na kwa sekondari wahamasishe umuhimu wa elimu na mahudhurio endelevu shuleni.

"Mkoa wetu tumepata aibu kubwa kwa kuwa namba mbili kwa utoro kati ya mikoa yote nchini, utoro huu hapa wilayani kwetu unachangiwa na umbali wa kwenda shuleni, hapa Busonzo watoto wetu wanasoma Runzewe ambapo ni mbali sana. Umbali huo unachangia utoro" alisisitiza Mhe. Biteko

Katika sherehe hizo zilizonakshiwa na Kaulimbiu ya mbio za mwenge kwa mwaka huu ambayo ni ‘Elimu ni ufunguo wa maisha, wekeza sasa kwa maendeleo ya Taifa letu.’ Waziri Mkuu alisema kuwa utoro wa wanafunzi wa Sekondari ni mkubwa zaidi kwa Mikoa husika kuliko shule za msingi. 

Mara baada ya uzinduzi Wa Mwenge huo wa Uhuru kabla ya kuelekea Mjini Dodoma kwa ajili ya shughuli za Bunge zinazotarajiwa kuanza kesho 3 Aprili 2018 Mhe Doto Biteko amezuru Kijiji cha Nampalahala kilichopo Kata ya Busonzo na kujionea jinsi ujenzi Wa maabara unavyoendelea.

Mara baada ya kubaini kuwa kuna upungufu wa matofali 10,000 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi huo, Naibu Waziri huyo amechagiza ujenzi huo kwa kuchangia gharama za ununuzi wa matofali hayo ili ujenzi huo ukamilike kwa wakati.

"Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatoa maelekezo ya kukomesha utoro naomba tukimbie kulitekeleza hilo na ninaomba wazazi tuhakikishe watoto wote wanakuwa shuleni ni aibu mno sisi kuwa vinara wa utoro". Aliongeza Mhe. Mbunge Na Naibu Waziri huyo.

Mhe Biteko amewaeleza wananchi hao jinsi ambavyo utoro kwa shule za sekondari Mkoani Geita umekithiri jambo ambalo limepelekea Mkoa huo kushika nafasi ya pili kwa utoro Kitaifa kwa asilimia 8.1, ambapo Mtwara imekuwa nafasi ya tatu kwa asilimia 6.4, Shinyanga asilimia 6.3 huku nafasi ya kwanza ikishikiliwa na Mkoa Wa Tabora kwa asilimia 9.7 

Aidha, Mhe Biteko ameonyesha kusikitishwa na takwimu za Mkoa Wa Geita kushika nafasi ya pili pia katika kwa utoro kwa shule za msingi kwa kwa asilimia 3.1 nyuma ya Mkoa Wa Rukwa unaoongoza kwa asilimia 3.2

Aliongeza kuwa anatamani kuona  Wilaya ya Bukombe inahakikisha inafikia viwango bora vya elimu. Serikali ya awamu ya tano inyoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli, imedhamiria kuboresha elimu katika ngazi zote nchini, kuanzia Elimu ya Awali hadi Elimu ya Juu hivyo wananchi wanapaswa kuitumia fursa hiyo kwa maendeleo ya wilaya hiyo na Taifa kwa ujumla aliwaomba pia wananchi wa  kata ya Busonzo kumuombea Rais Magufuli na kuunga mkono juhudi za serikali.
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa