Home » » JAJI MKUU AZITAKA MAHAKAMA MKOANI GEITA KUMALIZA KESI KWA WAKATI

JAJI MKUU AZITAKA MAHAKAMA MKOANI GEITA KUMALIZA KESI KWA WAKATI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 
Na Lydia Churi – Geita.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mheshimiwa Mohamed Chande Othman amezitaka Mahakama za mkoa wa Geita kuhakikisha zinamaliza kesi kwa wakati ili kutekeleza lengo lililowekwa na Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama jana mkoani Geita, Jaji Mkuu alisema Mahakama ya Tanzania ilijiwekea malengo ya kumaliza kesi katika mahakama zake kwa wakati kulingana na aina ya mahakama.

Alisema kwa mahakama za Hakimu Mkazi, mahakama za Wilaya pamoja na Mahakama za   Mwanzo lengo lilikuwa ni kumaliza kesi zote ndani ya mwaka mmoja ili kuwafanya wananchi kuendelea kuwa na imani na mahakama zao kwa kuwa ni zaidi ya asilimia 90 ya wananchi wanahudumiwa na mahakama hizo. 

Jaji Mkuu alisema kwa mahakama za Mwanzo ambazo ziko 970 nchini kote lengo lilikuwa ni kuhakikisha hazikai na kesi kwa zaidi ya miezi sita kwa kuwa ndizo mahakama zinazohudumia wananchi wengi zaidi.  

Alisema ili kuziwezesha Mahakama kutekeleza lengo walilojiwekea, tayari Mahakama ya Tanzania imeajiri Mahakimu wapya 107 ambao watasambazwa kwenye Mahakama zote za Mwanzo nchini kwa ajili yakwendakutoa huduma ya msingi ya mahakama ya kutenda haki kwa wananchi wa Tanzania.

Akizungumzia suala la utoaji wa nakala za hukumu, Jaji Mkuu amezitaka Mahakama za mkoa wa Geita kutoa nakala hizo mapema iwezekanavyo ili kutoa haki ya kukata rufaa kwa wananchi ambao hawakuridhishwa na hukumu walizopewa katika kesi zao.

Alisema Mahakama ya Tanzania itaongeza idadi ya Makatibu Mahususi na kuongeza vifaa katika Mahakama zake ili kuongeza kasi ya uchapaji wa nakala za hukumu. Alisema asilimia 80 ya bajeti inayotolewa kwa muhimili huo imetengwa kwa ajili ya kuendesha kesi katika mahakama za Mwanzo, Wilaya na zile za Hakimu Mkazi.

Jaji Mkuu anaendelea na zaira yake katika Mahakama Kuu kanda ya Mwanza ambapo anatembelea mikoa Mwanza, Geita na Mara ili kukagua shughuli za kimahakama katika kanda hiyo.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa