Home » » MSAFARA WA RC GEITA WAPATA AJALI

MSAFARA WA RC GEITA WAPATA AJALI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
KATIBU Tawala wa Mkoa wa Geita, Seveline Kahitwa, amejeruhiwa vibaya na kulazimika kukimbizwa katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, katika ajali iliyotokea juzi Kijiji cha Bugulula.
Katika ajali hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Geita (RC), Said Magalula, alipata majeraha madogo miguuni na mkono wake wa kushoto.
Viongozi hao walipata ajali hiyo walipokuwa katika msafara wakielekea katika Hifadhi ya Taifa ya Msitu wa Rwande katika Halmshauri ya Wilaya ya Geita, unaodaiwa kuvamiwa na wakulima na wafugaji.
Imedaiwa kuwa chanzo cha ajali hiyo, ni kusimama ghafla kwa gari la Mkuu wa Polisi Wilaya ya Geita, Busee Bwire, lenye namba PT 1998 kumkwepa mtoto John Haule (4) aliyekatisha ghafla barabarani.
Kitendo hicho kilifanya magari yaliyokuwa katika msafara huo, likiwemo la mkuu wa mkoa, katibu tawala mkoa, kamanda wa polisi mkoa na mkuu wa wilaya ya Geita kugongana ovyo na kusababisha majeruhi kwa baadhi ya viongozi hao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Joseph Konyo, alisema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa wazazi wa mtoto huyo ambao walimwachia kuvuka barabara, na kwamba kama sio uhodari wa dereva maisha ya mtoto huyo yangepotea.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali Teule ya Wilaya ya Sengerema, aliyetambulika kwa jina moja la Dk. Charles, alikiri kupokea majeruhi wa ajali hiyo kutoka Geita, lakini hakuwa na taarifa kama ni katibu tawala wa mkoa.
Kutokana na ajali hiyo, Magalula alilazimika kusitisha ziara hadi hapo itakapopangwa tena.
Msitu wa Rwande wenye ukubwa wa ekari 16,000, umevamiwa na wakulima na wafugaji tangu mwaka jana, huku wakitetewa na baadhi ya wanasiasa wanaotaka waruhusiwe kuendesha shughuli za kilimo na ufugaji katika msitu huo.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa