Home » » KERO ZISIVUNJE MUUNGANO

KERO ZISIVUNJE MUUNGANO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutoka Zanzibar, Juma Ali Khatibu amesema kero za Muungano haziwezi kuwa sababu ya kuvunja Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaliwa mwaka 1964.
“Dunia hivi sasa inaungana, nchi nyingi zinakuwa wamoja. Jambo la kufanya hapa ni Bunge la Katiba kuangalia kero zetu ni zipi katika Muungano halafu tukaziondoa,” alisema Khatibu.
Akizungumza mjini Dodoma jana, Khatibu alisema wajumbe wa Bunge hilo wanapaswa kuonyesha uzalendo katika kufikia uamuzi.
“Mimi ninachotaka kusema ni kuwa tumempata Rais muungwana sana na kwa kweli nampongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kuamua kwamba kabla hajaondoka madarakani tupate Katiba Mpya,” alisema Khatibu.
Khatibu alisema kitendo hicho ni cha kihistoria na kwamba Watanzania watamkumbuka kwa mwafaka wa kisiasa wa Zanzibar na sasa Katiba Mpya.
Khatibu alisema baadhi ya viongozi wa nchi za Afrika hawataki kuruhusu kuandikwa kwa Katiba Mpya mpaka kwanza waone damu imemwagika lakini Tanzania inaandika Katiba yake ikiwa katika mazingira ya amani.
Aliwasihi wajumbe wenzake waepuke kutazamana kwa misingi ya Uzanzibari na Ubara na badala yake, washikamane kwa masilahi ya taifa na wananchi kwa jumla.
“ Tanzania ni mfano wa kuigwa katika Afrika, nchi nyingi sana zinajifunza kutoka kwetu kwa hiyo, Katiba isitufanye tutengane. Kero za Muungano haziwezi kutufanya sisi tuvunje Muungano,” alisema.
Malalamiko ya kero za Muungano yamekuwapo kwa miaka mingi huku wanasiasa wakililia haja ya kuwapo kwa muundo mpya utakaotoa fursa sawa kwa pande mbili za Muungano.
Hata hivyo, Rasimu ya Pili ya Katiba inapendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu jambo ambalo linatazamiwa kuzua mvutano mkubwa wakati utakapofika muda wa kujadili Muungano kwenye Bunge la Katiba.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa