Home » » Asakwa kwa kunyonga mtoto

Asakwa kwa kunyonga mtoto

JESHI la Polisi mkoani Geita linamsaka Shija Hamisi (28), mkazi wa Kijiji cha Ibamba kwa tuhuma za kumuua mtoto wake mwenye umri wa wiki mbili kwa kumnyonga kwa wivu wa mapenzi.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Kamishina Msaidizi Mwandamizi, Leonard Paul, alisema kuwa mtuhumiwa huyo anaendelea kusakwa kwa kuwa alitoweka baada ya tukio hilo.
Alisema tukio hilo lilitokea Jumatano iliyopita na kwamba chanzo ni ugomvi wa kifamilia kati ya mtuhumiwa huyo na mkewe, Juliana Juma (20).
Inaelezwa Februari mwaka jana, Hamisi alikamatwa kwa tuhuma za wizi wa mifugo wilayani Biharamulo, Kagera na alipotoka mahabusu alimkuta mkewe akiwa mjamzito, hali iliyomtia shaka huenda mimba hiyo si yake.
Baada ya kujifungua Januari 22 mwaka huu, mtuhumiwa alidai mtoto aliyezaliwa si wake na inadaiwa siku ya tukio, mkewe alikuwa akipika jioni, na yeye alienda ndani alipokuwa amelala mtoto huyo na kumnyonga.
Taarifa hizo zinaeleza baada ya kumuua mtoto huyo kwa kumnyonga, alichukua baiskeli kama anatoka kidogo huku mkewe akiendelea kupika, lakini baada ya muda hakumsikia mtoto akilia ndipo alipoamua kwenda ndani na kukuta mtoto amenyongwa na kutupwa chini.
Kamanda aliwataka wananchi wa Mkoa wa Geita kuendelea kutoa ushirikiano ili kuwabaini watu wanaojihusisha na vitendo viovu, waweze kukamatwa na kufikishwa mahakamani.
“Nawaonmba wananchi wasichukue sheria mkononi wawalete watuhumiwa nasi tutawafikisha mahakamani,” alisema Kamanda Paulo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa