Home » » BUKOMBE HATARINI KUKUMBWA NA KIPINDUPINDU

BUKOMBE HATARINI KUKUMBWA NA KIPINDUPINDU

WANANCHI wa eneo la soko la chakula la mji mdogo wa Ushirombo, wilayani Bukombe, Geita, wapo hatarini kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na dampo la taka kufurika.
Diwani wa mji mdogo wa Ushirombo, Soud Ntanyagala  (CHADEMA), alibainisha hayo alipozungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kumalizika kikao cha baraza la madiwani cha Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe.
Alisema kutokana na hali hiyo anakusudia kuhamasisha mgomo kwa wananchi wa mjini huo ili kushinikiza halmashauri kuzoa taka hizo.
“Kwa sasa soko hili limejaa uchafu mwingi, halmashauri imekuwa ikichelewa kuzoa taka na sasa imefikia hatua mbaya, wapo wafanyabiashara wa mboga mboga na vyakula kwa maana nyingine kuna uwezekano wa wafanyabiashara na wateja wao kupatwa na magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu.
“Nimepiga kelele nimeshindwa, kilichobaki kwa sasa ni kuhakikisha nashawishi maandamano kwa ajili ya kushinikiza halmashauri ifanye haraka kuondoa taka hizo,” alieleza diwani huyo.
Mbali na hilo, alisema atahakikisha anapinga tabia ya kubadilisha matumizi ya fedha ambazo zimekusudiwa kufanya miradi mbalimbali lakini zinabadilishiwa matumizi.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Lilian Matinga, alisema atasimamia uamuzi wa madiwani wenye masilahi kwa wananchi wa wilaya hiyo.
“Nipo kwa ajili ya kusimamia maendeleo ya wananchi na sitakubaliana na kiongozi yeyote ambaye anataka kufanya halmashauri kama mali yake au kuisababishia hasara halmashauri kwa kushindwa kutumia fedha ambazo zimekusudiwa kutumika katika miradi mbalimbali,” alisema mkurugenzi huyo
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa