Home » » MAJAMBAZI YAUA,YAPORA FEDHA

MAJAMBAZI YAUA,YAPORA FEDHA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
NI kama sinema vile iliyochezwa na majambazi mawili katika mji wa Geita.
Majambazi hayo, juzi yaliuteka mji wa Geita kwa takribani dakika 15 kwa mtutu wa bunduki na kupora fedha huku wakala mkuu wa kutoa huduma za fedha kupitia mitandao ya simu za mkononi na wakala wa huduma ya CRDB, Gosbert Walwa, akiuawa kwa kupigwa risasi dukani kwake.
Tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 11 jioni mjini hapa na kuibua taharuki kubwa kwa wananchi kukimbia kunusuru maisha yao, huku baadhi ya wafanyabiashara wakifunga maduka kuhofia risasi zilizokuwa zikivurumishwa muda huo.
Majambazi hayo yalipora fedha kwenye ofisi ya Kampuni ya Blue Coast Investment Ltd na kwenye ofisi ya wakala wa usambazaji wa bia mjini Geita, Ignas Athanasi Inyasi.
Baada ya kufanya uporaji huo, majambazi hayo yaliondoka na kufyatua risasi barabarani na kulishambulia gari moja lililokuwa barabarani kabla ya kuingia dukani kwa wakala mkuu wa kutoa huduma za fedha kwa mitandao ya simu, Walwa, ambaye aliuawa nje ya duka lake.
Mmoja wa walioshuhudia tukio hilo, alisema watu hao waliingia ndani ya duka la Walwa na wakati wanatoka, walikutana naye mlangoni na kumpiga risasi iliyompata tumboni na kuanguka kisha kupoteza maisha hapo hapo.
“Hao watu walifika wakaegesha pikipiki yao nje, walikuwa wamevalia makoti meusi na kichwani walivaa kofia ngumu (Helmet), baada ya kumpiga Walwa (Wakala), walichukua pikipiki yao wakapiga risasi moja hewani,” alisikika mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo.
Shuhuda mwingine alisema tukio hilo limetokea umbali wa mita kama 50 kutoka zilipo ofisi za benki za NBC, NMB na Posta, zinazolindwa na askari polisi ambao walikuwa wakishuhudia sinema nzima ya tukio hilo bila kutoa msaada.
Mbali na kusababisha mauaji hayo, majambazi hayo yalimjeruhi kwa risasi Alex James (29), dereva wa Kampuni ya Dolfin raia wa Marekani na Albert Gasia (25) aliyekuwa kwenye gari alilokuwa akiliendesha James.
Muda mfupi baada ya tukio hilo, Mkuu wa Polisi Wilaya ya Geita, Busee Bwire, alifika eneo hilo kwa gari lake akiwa na askari zaidi ya watano, lakini majambazi hayo yalishatawanyika.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Prudensia Protas, alithibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kuongeza kwamba polisi wameanza msako na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa