Na Mwandishi wetu Geita yetu Blog.29/04/2014.
Hofu imezidi kutanda miongoni mwa jamii hasa kundi la
vikongwe baada ya vikongwe wanne kuuawa kikatili kwa kukatwa mapanga wilayani
Geita,matukio hayo yakihusishwa na imani za kishirikina na migogoro ya urithi
wa ng’ombe na mashamba katika kipindi cha wiki moja.
Matukio hayo yametokea siku chache baada ya mkuu wa
wilaya,Manzie Mangochie kutoa kauli mwishoni mwa wiki iliyopita ya kuwachukulia
hatua za kisheria viongozi wa maeneo yatakapotokea mauaji ya vikongwe.
‘’Tunayo matatizo ya mauaji ya vikongwe,hali hii ni Aibu na
hakuna mwenye mamlaka ya kuondoa uhai wa binadamu,kuua mtu wa Mungu?,nendeni
kuanzia sasa mkaimarishe ulinzi kwenye maeneo yenu likitokea tukio tutawakamata
viongozi wa eneo husika’’alisema dc kwenye kikao cha madiwani.
Kamanda wa polisi mkoani Geita Joseph Konyo,akithibitisha
jana(leo) kutokea kwa matukio hayo alisema tukio la kwanza lilitokea Aprili
23,mwaka huu saa 2 usiku katika kijiji cha Katoma baada ya watu wasiojulikana kufika
nyumbani kwa Kulwa Kapalata(67)kuomba maji kabla ya kumshambulia kwa kumkata
kwa mapanga kikongwe huyo na kusababisha kifo chake.
Aidha Konyo alisema Aprili 27,mwaka huu vikongwe watatu
waliuawa kwa nyakati tofauti katika vijiji vya Kagu,Butundwe na Kasamwa
wilayani hapa kwa kushambuliwa kwa mapanga na watu wasiojulikana.
Aliwataja Waliouawa kwamba ni,Joyce Dotto(70)mkazi wa
Butundwe ambaye aliuawa na watu wasiojulikana akiwa eneo la shule ya msingi
Chikobe akiwa njiani kurudi nyumbani akitokea kwenye Klabu ya pombe za
kienyeji.
Mwingine ni Yombo Petrol(50)Mkazi wa Kanyala Kasamwa,akiwa nyumbani
alivamiwa nyumbani kwake saa 1 usiku na watu watatu waliomshambulia kwa mapanga
sehemu za shingoni na mikono na kusababisha kifo chake kisha wauaji walichukua
ng’ombe wawili wakaondoka nao.
Hata hivyo ng'ombe hao walikutwa hatua chache kutoka nyumbani kwa kikongwe huyo wakiwa wamekatwa miguu yote na wauaji hao.
Katika tukio la tatu kikongwe mwingine aliyeuawa ni Kabula
Yohana(60)mkazi wa kitongoji cha Nchankungu kijiji cha Kagu,ambaye aliuawa
kikatili kwa kukatwa mapanga na kundi la watu wasiojulikana idadi yao na mara
baada ya kufanya mauaji hayo waliotoweka kusiko julikana.
Katika kipindi cha mwaka jana vikongwe 15 waliuawa kikatili mkoani
Geita kwa imani za kishirikina na migogoro ya urithi wa mashamba na mifugo katika
wilaya za Geita,Chato na Bukombe.
Kufuatia maujai hayo baadhi ya vikongwe wanaishi kwa hofu
kwenye familia zao kutokana na kutuhumiwa kuhusika katika vifo vya baadhi ya
ndugu,majirani na jamaa zao baada ya
kwenda kupigiwa ramli kwa waganga wa kienyeji kutaka kujua waliohusika na vifo
vya ndugu zao.
0 comments:
Post a Comment