Mwanamke mjamzito mkazi wa kijiji cha
Nyamalembo wilayani Geita, Magdalena Kyaruzi (26) , ameuawa kikatili nyumbani
kwake kwa kukatwa panga shingoni na mtu anayesadikiwa kuwa mgeni.
Mwanamke huyo
alikuwa na ujauzito wa miezi minne, ambapo mumewe ni mfanyakazi wa kampuni ya
Moolman, inayojishugulisha na uchimbaji dhahabu katika mgodi wa Geita (GGM).
Kamanda wa
Polisi mkoani Geita , Leonard Paulo , alithibitisha kutokea kwa tukio hilo. "Ni kweli tukio
hili lipo na lilitokea juzi saa 3:30 asubuhi, ambapo mtu ambaye hadi sasa
hajulikani jina wala sura yake alifika nyumbani kwa mama huyu kisha kufanya
ukatili huo wakati mumewe akiwa kazini,"alisema.
Alisema muuaji huyo kabla
hajafanya ukatili huo, alifika nyumbani hapo na kubisha hodi alipokaribishwa
ndipo alianza kumkata mapanga sehemu ya kisogoni, kichwani na kufa papo hapo.
Alisema, mara
baada ya kutimiza azma yake hiyo, muuaji huyo alitoweka na simu ya marehemu, na
kuwa taarifa za kiintelijensia zinaeleza kuwa mtu huyo aliwahi kufika nyumbani
hapo mwezi mmoja uliopita.
"Uchunguzi
wetu wa awali umebaini kuwa mwezi mmoja uliopita wakati mumewe akiwa hayupo,
alifika hapo na kufanya mazungumzo naye jambo linaloonesha kuwa walikuwa
wanafahamiana," alisema.
Alisema, jeshi hilo bado linaendelea na
uchunguzi zaidi kubaini chanzo chake na kwamba hakuna mtuhumiwa anayeshikiliwa
kutokana na mauaji hayo.
0 comments:
Post a Comment