Home » » MAGUFULI AWAAGA WAPIGAKURA WAKE CHATO.

MAGUFULI AWAAGA WAPIGAKURA WAKE CHATO.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli

Waziri wa Ujenzi,  Dk. John Magufuli, amewaaga rasmi wakazi  wa Chato mkoani Geita, akisema hatagombea tena ubunge katika jimbo hilo  baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumteua kuwa mgombea wake wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini Oktoba 25, mwaka huu.
 
Mbali na kuwaaga wakazi  hao, Magufuli ameahidi kuendelea kushirikiana na wananchi ili   kuhakikisha Tanzania inapata maendeleo haraka.
 
Aliwaambia wakazi hao kuwa atakapochaguliwa kuwa Rais katika uchaguzi huo utakavishirikisha vyama vya siasa vya upinzani nchini, atakuwa msikivu na mwenye kukubali kuelekezwa na marais waliotangulia.
 
"Ndugu zangu nawashukuru kwa kuniamini na kunipa nafasi ya kuwatumikia kwa miaka 20 nikiwa mbunge wenu...tumefanya kazi nzuri naamini kila mmoja wenu anajua hilo," alisema na kuongeza kuwa:
 
"Lakini pia nilipofika hapa kuomba udhamini wa nafasi ya kuteuliwa na CCM kugombea urais mliniahidi na kuniombea sana ili nifanikiwe na hatimaye imekuwa." alisema. Alisema anachoweza kuwaambia ni kuwashuri na kusisitiza kuwa hatawaangusha atakapoingia Ikulu.
 
"Ninachoweza kusema kwenu  asanteni sana, naahidi kutowaangusha nitawatumika Watanzania wote pasipo kujali itikadi za vyama vyenu, dini, kabila kwa kuwa maendeleo hayana chama. Kazi niliyokabidhiwa na chama changu ni kubwa na nitakuwa msikivu kwa kuwa chama chetu kinao wazee wengi wenye bussara ukianzia Mzee mkapa, Mwinyi, Kalume, Jakaya na wengine wengi."
 
Wakati Dk Magufuli akiwaaga wakazi hao waliokuwa wamefurika kwenye viwanja vya kituo cha zamani cha mabasi wilayani Chato, kumsikiliza walisikika wakisema yeye ndiye mkombozi wa Tanzania.
 
AZUNGUMZIA UKANDA
Magufuli ambaye alipokelewa kwa mbwembwe katika jimbo hilo, awali alisema kuwa wakazi wa Kanda ya Ziwa wasitegemee katika uongozi wake atafanya upendeleo.
 
Alisema hatakuwa na upendeleo wa kikanda katika uongozi wake huku akisisitiza  kipaumbele kikubwa ni kuhakikisha ajira inapewa kipaumbele kwa vijana.
 
“Nitahakikisha natenda haki sawa kwa wote bila kuangalia huyu ni mwana CCM, Ukawa, ujimbo ama ukanda, lengo ni kuleta maendeleo kwa wote na wala wananchi wasitegemee wapo nitakaowabeba,” alisema Dk. Magufuli.
 
Alisema maendeleo hayana chama fulani, bali yapo kwa wananchi wote ambao ni wazawa wa nchi hii hivyo wale wanaoamini Rais kutoka kanda ya ziwa ataonyesha upendeleo, amefilisika kimawazo.
 
 "Magufuli ni wenu wenyewe mlimchagua kuwatumika Watanzania na kwa kuwa hamkukosea kumchagua kuwa Mbunge wenu, pia serikali iliona kuwa hili ni jembe na kumteua kuwa Waziri kwa kipindi chote cha utumishi wake," alisema Nape na kusisitiza kuwa:
 
"Kana kwamba haitoshi CCM kimeendelea kuridhishwa na uwajibikaji wake na sasa kinampa ridhaa ya kugombea urais."
 
Baadhi ya wakazi wa jimbo hilo, waliliambia NIPASHE kuwa wamefurahishwa na CCM kumteua Magufuli kuwa mgombea urais kinyume na matarajio ya wengi. 
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Geita Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa